Dini ni mfumo wa maishani

Dini ni mfumo wa maishani

Monday, January 10, 2011

SIASA NA MFUMO WA DINI MAISHANI

Mussa Juma, Arusha
MAASKOFU wa makanisa ya Kikristo mkoani Arusha, wametoa tamko la pamoja la kutomtambua Meya wa Jiji la Arusha aliyeteuliwa na CCM na kuweka bayana kwamba "hawatampa ushirikiano".Walitoa tamko hilo jana wakati wakilaani hatua ya polisi mkoani Arusha, kutumia nguvu kupita kiasi katika kuvunja maandamano ya amani ya Chadema na hivyo kusababisha vifo vya watu watatu na kujeruhi wengine zaidi ya 20.


Akisoma tamko la umoja wa viongozi wa dini ya kikristo mkoani Arusha, Askofu Mkuu wa Kanisa Katoliki, Jimbo Kuu la Arusha, Josephat Lebulu alisema Jeshi la Polisi ndilo lilikuwa chanzo cha vurugu hizo.

Tamko la maaskofu hao limekuja siku moja tu tangu Serikali kupitia kwa Waziri wa Mambo ya Ndani, Shamsi Vuai Nahodha atoe tamko kwamba vurugu zilizotokea Arusha ni tatizo la kisiasa ambalo pia litapaswa kushughulikiwa kisiasa.

“Wote tunapaswa kulinda amani yetu. Tunapaswa kutuliza hali ya Arusha. Kilichotokea Arusha ni mgogoro wa kisiasa, tutautatua pia kisiasa,” alisema Nahodha alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari, juzi jijini Dar es Salaam.



Kuhusu uwezekano wa kutengua matokeo ya umeya Arusha, suala ambalo pia Chadema wanalilalamikia, Naodha alisema “Sina uhakika kama tatizo la msingi lililopo Arusha linatokana na Umeya. Lakini katika mazungumzo tukibaini kuwa hilo ndiyo tatizo basi tutalifanyia kazi.”

Lakini jana Askofu Lebulu alisema, "Sisi kama viongozi wa dini hatuwezi kushirikiana na mtu ambaye hakushinda kihalali, kuna mtu alipiga kura si diwani wa Arusha, Chadema hawakushirikishwa na pia taratibu na kanuni za uchaguzi huo zilikiukwa".

Maskofu hao walisema chanzo cha vurugu hizo ni hila zilizofanywa na baadhi ya watu ili kumsimika Meya wa jiji la Arusha, Gaudence Lyimo wa CCM.

Kwa mujibu wa malalamiko ya Chadema, mbunge ambaye hakustahili kupiga kura ni wa viti maalum CCM Mkoa wa Tanga na Katibu wa CCM Mkoa wa Arusha, Mary Chatanda ambaye alipiga kura kama diwani wa Arusha.

Katika tamko lao, maaskofu hao walieleza kuwa kama Serikali inataka kutunza amani inatakiwa kuhakikisha haki inatendeka kwani haki na amani ni vitu visovyotenganishwa.

"Serikali ina wajibu na dhamana ya kutunza watu wake, hatukubaliani na mtu yoyote ambaye anaamua kutekeleza mauaji kwa wengine," alisema Leburu.

Hata hivyo, maaskofu hao, walitoa wito kwa vyama vya siasa kukubali kushindwa na kukosolewa, lakini wakasisitiza kuwa wito huo hauna maana kwamba wakae kimya pale wanapotendewa vibaya.

Maaskofu hao pia waliigeukia Chadema wakisema haiwezi kukwepa kuwa sehemu ya chanzo cha vurugu hizo kwa sababu ilikuwa na uwezo wa kuwazuia wafuasi wake kutoandamana ili kutii amri iliyotolewa na polisi.

"Lakini pia Chadema walitakiwa kufanya kila jitihada kuwajulisha wafuasi wake kutoandamana licha ya kuzuiwa kufanya maandamano hayo muda mfupi kabla ya kuanza," alisema Askofu Lebulu.

Kutokana na vurugu hizo, Maaskofu hao walisema Serikali inapaswa kushughulikia mgogoro wa Arusha kwa hekima, busara na uwazi kwani ni dhahiri kuwa taratibu za kumchagua Meya zilikiukwa.

Askofu Lebulu pia alisema Serikali inapaswa kuchukua tukio la Arusha kama jambo la kitaifa na kufanya jitihada za kulishughulikia haraka na kwa amani.

Naye, Askofu Thomas Laizer wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri (KKKT) Dayosisi ya Arusha, alisema kutokana na polisi kutumia nguvu kubwa, hawatasitisha mahusiano yao na Serikali pamoja na polisi kwa sababu kufanya hivyo ni kujitenga na majukumu.

"Ushirikiano wetu hauwezi kukatishwa na vurugu hizi kwani huwezi kutatua tatizo kwa kulikwepa," alisema Askofu Laizer.

Katika kikao hicho, pia walihudhulia Askofu Martin Shao wa KKKT Dayosisi ya Kaskazini, na maaskofu wa makanisa na Kipentekoste ya mkoani Arusha.

Wakati huo huo, Meya anayelalamikiwa Gaudence Lyimo amesema hafikirii kujiuzulu katika nafasi hiyo kwani amechaguliwa kihalali na kwa kufuata taratibu.

Akizungumza na Mwananchi kwa simu jana, Lyimo alisema kitendo cha Chadema kuandamana na watu kufariki kutokana na mgogoro wa yeye kuchaguliwa hakuwezi kumsukuma ajiuzulu.

"Mimi kwa nini nijiuzulu? Nimechaguliwa na madiwani kwa kufuata sheria na hao waliandamana mimi siwezi kuwazungumzia kuwa waliandamana kwa ajili yangu," alisema Lyimo.

Wafuasi wa Chadema, wakiwepo wabunge na viongozi wa Kitaifa, Mwenyekiti Freeman Mbowe na Katibu Mkuu, Dk Willibrod Slaa walifanya maandamano Alhamisi iliyopita licha ya kuzuiwa na polisi makao makuu wakati ambapo yalikuwa yamepewa kibali na Polisi mkoa wa Arusha.

Katika maandamano hayo, watu watatu wamefariki ambao ni Denis Shirima (25), Mwita Marwa (24) na Ismail Omar (40) huku wengine zaidi ya 20 wakijeruhiwa 16 kwa kupigwa risasi.


Dini nchini Tanzania


Msikiti huko mjini Moshi, Tanzania.



Kanisa huko mjini Songea.




Dini za wananchi wengi wa nchi ya Tanania ni Uislamu, Ukristo na dini asilia za Afrika (dini za jadi). Nje ya hao wako wachache wanaofuata Uhindu, Usikh na dini nyingine na mara nyingi hawa ni wahamiaji katika nchi au wamezaliwa katika vikundi vyenye asili ya uhamiaji kutoka nje.

Siasa ya serikali na dola ni kutokuwa na dini rasmi. Katiba inatoa uhuru wa dini, na serikali inaheshimu haki hii kwa vitendo.




Dini za jadi

Hadi vizazi vichache vilivyopita idadi kubwa ya wakazi wa eneo la Tanzania la leo walifuata dini asilia za Kiafrika. Wakati wa karne ya 19 Uislamu ulipatikana kwenye pwani hasa katika mazingira ya mji ya Waswahili na pia kwenye vituo vya biashara vya Waswahili kando la njia ya misafari kuelekea eneo ya maziwa makubwa kutoka pwani. Tangu katikati ya karne ya 19 Wamisionari Wakristo wa kwanza walianza kufika kwenye pwani na kujenga vituo vyao barani.

Wakristo na Waislamu walikuta kote wafuasi wa dini za jadi. Polepole wengi wao walihamia upande wa dini hizi kubwa. Lakini desturi na ibada mbalimbali za kijadi ziliendelea kufuatwa na sehemu ya Wakristo na Waislamu wapya hadi leo.

Uislamu katika Tanzania
Asilimia tisini na saba ya wakazi wa funguvisiwa vya Zanzibar ni Waislamu. Kwa upande wa Tanzania bara, jumuia za Kiislamu huzingatiwa sana katika maeneo ya pwani, na baadhi ya Waislamu wanaoishi katika maeneo ya mijini huko bara. Kati ya asilimia 80 na 90 ya idadi ya Waislamu nchini ni Sunni wa madhhab ya Shafi'i. Wasunni wachache wenye asili ya Kiasia ni Wahanbali kuna pia wafuasi Maliki na Hanbali ambao ni asili wa Yemen.

Washia ni wachache wengi wao wenye asili ya Kiasia au Arabuni. Kundi linaloonekana zaidi ni Ismaili au wafuasi wa Aga Khan ambao ni kitengo cha Washia Sabi'a. Kitengo kingine cha Shia hii ni Bohra. Wafuasi wa Shia Ithnasheri (Imami) si wengi lakini wanapata usaidizi kutoka Uajemi ambako imani ao ni dini rasmi. Wafuasi wa Ibadiyya wana asili ya Oman.

Kundi la Ahmadiyya liko wanajitahidi kupata waumini lakini bila mafanikio makubwa.

Ukristo katika Tanzania

Idadi ya madhehebu ya Kikristo inajumlisha Kanisa Katoliki, Waprotestanti wa aina mbalimbali (Wapentekoste, Waanglikana, Walutheri, Wasabato, Kanisa Jipya la Kitume n.k.), Waorthodoksi na Waorthodoksi wa Mashariki wachache, mbali ya Wamormoni na Mashahidi wa Yehova.

[hariri] Dini nyingine
Kuna Watanzania wanaofuata Uhindu na Usikh hasa raia wenye asili ya Asia. Imani ya Baha'i nayo imeanzishwa katika maeneo kadhaa ya nchi.

Takwimu ya dini

Sensa ya 1967

Takwimu ya dini nchini Tanzania kwa sasa haipatikani kwa sababu maswali kuhusu dini yaliondolewa na serikali katika sensa baada ya mwaka 1967. Sensa ile ya tarehe 27 Agosti ilihesabu wafuasi wa dini za jadi kuwa 34.3%, Wakristo 33.5% na Waislamu 31.4%, mbali na wengineo 0.8%.[1]

Namba zenye athira ya kisiasa
Tangu mwaka ule swali la takwimu ya kidini Tanzania limejadiliwa sana inaonekana ni swali lenye uzito wa kisiasa pamoja na upande wake wa kitaalamu.

Kwa miaka mingi makadirio ya kawaida yalikuwa Watanzania ni theluthi 1 wafuasi wa dini za jadi, theluthi 1 Waislamu na theluthi 1 Wakristo.[2]

Lakini ni wazi ya kwamba dadi ya wafuasi wa dini za jadi imeendelea kupungua. Baadhi ya viongozi na wanaelimu-jamii wanakadiria kwamba jumuia za Kikristo na Kiislamu zipo sawa tu kwa ukubwa, zote huhesabiwa kiasi cha asilimia 30 hadi 40 kwa idadi ya wakazi, na waliosalia ni waumini wa imani zingine, dini za jadi, na wale wasio na dini kabisa.

Lakini wataalamu wengine wanasema uwiano huo unashikiliwa kisiasa kwa sababu uhusiano kati ya Wakristo na Waislamu ni jambo la siasa ya taifa kwa hiyo makadirio yanaelekea kutaja uwiano sawa kati ya pande hizi mbili.[3]

[hariri] Mifano ya makadirio mbalimbali
Kwa hiyo namba zote kuhusu takwimu ya dini nchini Tanzania ni makadirio tu hakuna namba za kutegemea. Vyanzo vinavyotaja namba vinatofautiana sana mara nyingi kufuatana dini ya wahariri.

No comments:

Post a Comment