Dini ni mfumo wa maishani

Dini ni mfumo wa maishani

Saturday, November 27, 2010

Padri anayedaiwa kulawiti kortini


Daniel Mjema, Moshi
HATIMAYE Padri Stanslaus Msafiri Salla (70) wa Parokia ya Kilema ya Kanisa Katoliki Jimbo la Moshi mkoani Kilimanjaro, amefikishwa mahakamani akikabiliwa na shtaka la kumlawiti kijana mwenye umri wa miaka 16.

Padre Salla ambaye alipelekwa mahakamani jana kwa njia ambayo polisi walisema ni ya “kistaarabu”, aliachiwa kwa dhamana baada ya kutimiza masharti ya kuwa na wadhamini wawili waliomdhamini kwa Sh10 milioni kila mmoja.
Ingawaje hati ya mashtaka iliwasilishwa kortini na polisi saa 3:00 asubuhi na kufunguliwa na kupewa namba 743/2010, lakini padre huyo alifika mahakamani hapo saa 5:30 kwa mazingira yaliyoibua maswali mengi kuliko majibu.

Mshtakiwa huyo aliingia mwenyewe jengo la mahakama na polisi mwenye cheo cha Koplo namba 5397, alimwelekeza asiingie mahabusu bali aende moja kwa moja kukaa kwenye benchi la hakimu aliyepangiwa kesi hiyo.
Akimsomea shtaka linalomkabili, Wakili wa Serikali, Abdallah Chavulla, alidai mahakamani kuwa, Oktoba 30, mwaka huu majira ya usiku eneo la Kilema Leso, Padre huyo alimuingia kinyume cha maumbile kijana mwenye umri wa miaka 16.

Alidai kuwa, kitendo kilichofanywa na Padre huyo kilikuwa ni kosa chini ya kifungu namba 154 (1) (a) cha sura namba 16 cha kanuni ya adhabu kama kilivyofanyiwa marekebisho na Bunge mwaka 2002.

Chini ya kanuni hiyo, anayepatikana na hatia atatakiwa kutumikia kifungo cha miaka 30 jela isipokuwa kama mshtakiwa atakuwa amemfanyia kitendo hicho mtoto chini ya miaka 10 basi, adhabu yake ni kifungo cha maisha.
Hakimu Mkazi Mfawadhi Mkoa wa Kilimanjaro, Simon Kobelo, alisema dhamana ya mshtakiwa huyo ilikuwa wazi na ndugu waliojitokeza mahakamani hapo wakiwamo baadhi ya mapadre, walifanikiwa kutimiza masharti hayo.

Wakati huohuo, Kamanda wa Polisi Mkoa Kilimanjaro, Lucas Ng’hoboko, amekanusha kumlinda kwa namna yoyote mtuhumiwa huyo akisema hapaswi kunyooshewa kidole kwani, yeye ni mtawala sio mpelelezi wa makosa ya jinai.
“Naambiwa natumia ukatoliki wangu kumlinda Padre, kwanza mimi ni mtawala tu sio mpelelezi,” alisema Kamanda Ng’hoboko na kuongeza kuwa, uandaaji mashtaka sasa unafanywa na ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

Ng’hoboko alifafanua kuwa, taarifa kwamba fomu ya polisi (PF3) iliyopelekwa kwa mwanasheria wa serikali sio halisi, amezisoma kwenye vyombo vya habari na kuwataka wenye nakala halisi kuiwasilisha kwake ifanyiwe kazi

No comments:

Post a Comment